Blogu hii imedhaminiwa na Simba Video Coach

Blogu hii imedhaminiwa na Simba Video Coach
Kwa usafiri wa Dar es salaam, Morogoro, Dodoma na Arusha, safiri kwa raha na Simba Mtoto Luxury Coach

Tuesday, February 7, 2012

SHIRIKA LA MASUALA YA HAKI ZA WATOTO NA SANAA KUFANYA KAMPENI KATA YA USAGARA KUELIMISHA JAMII HAKI ZA WATOTO

MKURUGENZI MTENDAJI WA SHIRIKA LA UNITE TANZANIA CHILDREN LINALOSHUGHULIKA NA MASUALA YA AFYA YA MTOTO NA SANAA BI IRENE RAJAB MHANDO

MKURUGENZI WA SHIRIKA LA UNITE TANZANIA CHILDRENBI IRENE MHANDO

KATIBU WA SHIRIKA HILO BI DORO EZEKEL NTUMBO AKIWA KATIKA MAHOJIANO NA MWANDISHI WA HABARI HIZI KATIKA OFISI YAO ILIYOPO KATIKA JENGO LA READ CROSS

Na mzee wa Bonde,Tanga
SHIRIKA la Unite Tanzania linalojihusisha na afya ya mtoto na sanaa, limeandaa warsha kwa watendaji na wananchi katika kata ya Usagara Jijijini Tanga yenye lengo la kuijengea uwezo jamii kuhusu masuala yanayohusu haki mbalimbali za watoto ili waweze kuzitekeleza katika familia.

Sanjari na hilo, shirika hilo litaendesha kampeni kwa kufanya shughuli mbalimbali ikiwemo mabonanza ya watoto kwa kipindi cha miezi sita lengo likiwa kuhakikisha inapambana na vitendo vinavyowakosesha raha na haki watoto.

Mkurugenzi Mtendaji wa shirika hilo, Bi Irene Mhando, akizungumza na waandishi wa habari mjini hapa jana, alisema kuwa lengo la mradi huo uliofadhiliwa na mtandao wa mashirika ya kiraia ya Foundation For Civil Society, alisema kwa kipindi cha miezi sita watajikita katika kata hiyo kuzungumzia kwa undani haki anazostahili kupata mtoto na vile vile kutambua vipaji vyao.

Alitaja makundi ambayo watakutana nayo katika kipindi hicho kuwa ni pamoja na watendaji wa mitaa, madiwani, polisi na wananchi wa kawaida katika mitaa mbalimbali ya kata hiyo ambapo wanatarajia kwamba itawajengea uwezo wa kutambua kwa nini jamii inapaswa kuwalea watoto kwa mtizamo mpana.

"Shirika litaendesha mradi wa kampeni ya haki ya mtoto katika kata ya usagara, kwa kipindi cha miezi sita watazungumza na wananchi, watendaji, polisi na makundi mengine ya jamii ili kuhakikisha malengo ya kuijengea uwezo jamii yanatimia ipasavyo na watoto wanaishi kama watu wengine," alisema Mkurugenzi huyo.

Kwa upande wake, Katibu wa shirika hilo, Bi Doro Ntumbo, akijibu suala la kwanini wamechagua kata ya Usagara na siyo kata nyingine za Jiji hilo, alisema kuwa kata hiyo imekuwa na matukio mengi ya unyanyasaji wa mtoto hivyo kuendesha kampeni katika kipindi hicho kutasaidia kuongeza uelewa kwa jamii na matukio hayo mwisho wa siku kupungua.

"Ukitazama malengo ya mradi huu, kuwaongezea uelewa jamii kuhusu sera ya mtoto ya mwaka 2008, kubadilisha tabia za watu kuhusu namna wanavyotakiwa kuwapa haki watoto...Sasa kata ya Usagara tumeonelea tuanze nayo kwa vile masuala ya unyanyasaji yamekuwa yakikithiri hivyo kufika kwetu tutasaidia maana pia tutaunda mabaraza ya watoto, hii itasaidia kupunguza matukio ya ukiukwaji wa sheria za haki za mtoto," alisema Bi Ntumbo.
 


Friday, February 3, 2012

MAHARAMIA WACHOMA MOTO BOTI YA UVUVI KIGOMBE

MKUU WA MKOA LUTENI (MSTAAFU) CHIKU GALLAWA (mwenye kilemba) AKIMNYOOSHEA KIDOLE MKUU WA WILAYA YA MUHEZA BW. METHEW NASEI KWAMBA AHAKIKISHE WATU WALIOCHOMA MOTO BOTI YA UVUVI KATIKA MWAMBAO WA KIGOMBE WANAPATIKANA HARAKA.

WANANANCHI WA KIGOMBE WAKIMSIKILIZA MKUU WA MKOA. WA KWANZA KULIA NI MSAIDIZI WA MKUU WA MKOA BW. JOSEPH SURA.

BOTI YENYEWE AMBAYO IMECHOMWA MOTO NA MAHARAMIA

MKUU WA MKOA WA TANGA MH GALLAWA AKIWA NA VIONGOZI WA WILAYA YA MUHEZA NA KIJIJI CHA KIGOMBE WALIPOMTEMBEZA KWENYE MWAMBAO WA PWANI KUONA ENEO LILILOHIFADHIWA KWA AJILI YA SAMAKI AINA YA SILIKANTI.


Na Mzee wa Bonde,Muheza
MAHARAMIA wanaoendesha uvuvi haramu katika mwambao wa bahari ya Hindi mkoani Tanga, wameichoma moto boti ya doria inayomilikiwa na Taasisi ya Hifadhi ya bahari ya Silikanti iliyopo katika kijiji cha Kigombe wilayani hapa.

Kuchomwa kwa boti hiyo iliyokuwa ikielea baharini katika eneo hilo la Kigombe, kunatokana na dori ya mara kwa mara inayofanywa na taasisi hiyo kwa ajili ya kuwasaka maharamia wanaoendesha uvuvi haramu wa kutumia mabomu na nyavu ndogo zisizoruhusiwa, kumeelezwa kwamba ndiko kuliwapa hasira maharamia hao, wakachukua maamuzi hayo.

Mwenyekiti wa kijiji cha Kigombe Bew. Mwambi Haji alimweleza Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Luteni (Mstaafu) Chiku Gallawa aliyefika katika kijiji hicho kupata maelezo ya kuchomwa kwa boti hiyo, alisema tukio hilo lilitokea hivi karibuni na hadi sasa hakuna mtu yeyote aliyekamatwa kuhusiana na tukio hilo.

Mhifadhi wa bahari ya Silikanti Bw. Sylevester Kazimoto alisema katika kipindi cha mwaka uliopita waliendesha doria 192 za baharini na nchi kavu iliyohusisha vyombo vya dola ambayo iliwezesha kukamatwa kwa wavuvi haramu wapatao sita.

Alisema pamoja na kuwakamata wavuvi hao pia walikamata vifaa vinavyotumika kwa uvuvi huo ikiwemo baruti 29, bunduki 17 za kuulia samaki, mitungi 31 ya kuzamia, makokoro 94, nyavu za utale 11 na samaki wa baruti kilo 124.

Akizungumza katika mkutano na wananchi waliofika katika ofisi ya hifadhi hiyo Mkuu wa Mkoa alisema kuwa kila wananchi analojukumu kubwa la kulinda na kuhifadhi rasilimali za bahari hivyo akawataka wataalamu wa hifadhi hiyo wakishirikiana na serikali ya kijiji kuandaa mpango wa kuorodhesha wavuvi wote na boti zao kisha kuziandika namba.

Alisema suala la uvuvi haramu hivi sasa linatakiwa kupigwa vita baada ya muda mrefu nchi yetu kuliacha bila kuwachukulia hatua watu wanaoendesha uvuvi haramu ambao licha ya kuharibu mazingira pia wanaleta matatiz ya kiafya kwa kuvua samaki wa aina hiyo.

Hata hivyo, mjumbe wa serikali ya kijiji hicho Bw. Hassain Bakari almtaka mkuu huyo wa mkoa kuingilia kati suala la wavuvi haramu kukamatwa kisha kesi zao kuishia hewani kwa maana ya polisi na mahakamani hatua ambayo inasababisha wavuvi hao kutawala mwambao wa bahari kwa kuendesha vitendo hivyo wakiamini kwamba, wakikamatwa kesi zao watazimaliza.

Thursday, February 2, 2012

MPIGA PICHA MAARUFU MKOANI TANGA ELIAS NGOSWE, AGONGWA AKIPIGA PICHA KWENYE MAHAFALI

Mmoja wa majeruhi waliogongwa na gari lenye namba T489 AGJ aina ya Toyota Bw. Elias Ngole almaarufu Ngoswe ambaye ni mpiga picha maarufu mkoani Tanga, aliyefika kwenye mahafali ya kidato cha sita katika shule hiyo ya Korogwe Girls akiwa amepakiwa kwenye bajaj kukimbizwa katika hospitali ya Magunga kwa matibahu.

Mwanafunzi Renata Renatus anayesoma kidato cha sita katika shule hiyo, akiwa katika hospitali ya Magunga wilayani Korogwe akihudumiwa na muuguzi alipofikishwa katika hospitali hiyo.

Gari lililosababisha ajali likiwa limebenuliwa ili kuwatoa majeruhi wa ajali hiyo ambayo imeleta usumbufu mkubwa kwa wanafunzi na wazazi waliofika.

Mkuu wa wilaya ya Korogwe (mwenye suti nyeusi) akiwa amemshika mwanafunzi Kibibi Mmasa (19) ambaye ndiye aliyeendesha gari hilo kwa kuliweka gea kisha gari hilo kurudi nyuma na kuwagonga wanafunzi wenzake na kuwasababisha majeraha makubwa 

Mwanafunzi Zahra Jumanne (19) akipelekwa wodini baada ya kupatiwa matibabu mwanafunzi huyo ni mmoja ya wahitimu walioumia sana.

Mwanafunzi Nancy James akiwa amelazwa katika hospitali hiyo ya Magunga akipatiwa matibabu na wauguzi wa hospitali hiyo.
Na Mzee wa Bonde,Korogwe
VILIO, majonzi na huzuni vilitawala leo asubuhi katika shule ya sekondari ya Wasichana Korogwe, kufuatia wanafunzi wapatao saba na mpiga picha mmoja wa kujitegemea, kujeruhiwa vibaya kwa kugongwa na gari lililokuwa likichezewa na mmoja ya wahitimu wa kidato cha sita aliyeweka gia ya kurudi nyuma na kisha gari hilo, kuwagonga wahitimu hao.

Tukio hilo lililotokea majira ya saa 10:20 asubuhi katika shule hilo, baada ya mwanafunzi mmoja Kibibi Mmasa anayesoma kidato cha sita shuleni hapo, kuingia katika gari la kaka yake lenye namba za usajili T489 AGJ ambaye alifika kushuhudia mahafali hayo, aliweka gia hiyo kisha gari hilo kurudi nyuma kwa mwendo kasi wa kilomita 120 kwa saa na kuwaparamia wahitimu hao waliokuwa wamejikusanya vikundi.


Wanafunzi waliojeruhiwa na hali zao kuelezwa zipo katika hali mbaya ni Zahra Jumanne (19) na mpiga picha wa siku nyingi Bw. Elias Ngole 'Ngoswe', wengine ni Renata Renatus (25), Sophia Godfrey (19), Victoria Mtwale (19), Nancy James (19) na Mwanamkonda Kapunda (19) ambao wote wanasoma kidato cha sita na ambao walikuwa wakitarajia kufanya mahafali ya kumaliza shule.


Mwandishi wa habari hizi alishuhudia gari hilo likiendeshwa na mwanafunzi huyo likitembea kwa kasi kurudi nyuma na kuanza kumgonga mpiga picha huyo ambaye alikuwa akizungumza na Mwandishi wa ITV na Redi One Bw. William Mngazija ambaye baada ya kuliona gari hilo aliruka pembeni lakini mwenzake alishindwa na badala yake gari hilo lilimgonga kisha kunasa chini yake na kuburuzwa hadi kiasi cha mita 30 gari hilo lililopogonga mti na kusimama.


Baada ya kugongwa mpiga picha huyo liligonga wanafunzi wengine ambao walikuwa wamejikusanya wakibadilishana mawazo namna watakavyosherehekea mahafali yao ambayo mgeni rasmi alikuwa ni Mkurugenzi wa benki ya posta nchini Bw. Sabasaba Moshingi ambapo mmoja Zahra aligongwa vibaya na kunasa chini ya gari hilo ambapo gari hilo lilipinduliwa ili kumnasua huko chini akiwa amevunjika miguu na kupata jeraha kubwa kichwani.


"Kaka alinituma mle ndani ya gari wakati nikichukua mzigo aliyonituma ghafla nikaona gari linakwenda, nikawa sijui kinachoendelea nikasikia makelele wenzangu wanapiga huko nje huku nikiwa nimekanyaga mafuta," alisema Kibibi huku akisihi viongozi wamweche kaka yake ambaye alishikiliwa na polisi kuhusiana na tukio hilo. Kaka yake ni Hussein Mmasa.


Akizungumzia tukio hilo, Bw. Mngazija alisema kama si kupata ujasiri kuwa kusogea kulipisha gari hilo pengine naye angekuwa miongoni mwa watu waliojeruhiwa lakini ana mshukuru mungu kukwepa ajali hiyo.


"Nilikuwa nasalimiana na Ngoswe hatujaonana muda mrefu, sasa ghafla nikaliona gari linakuja kwa kasi nikaruka na kumuacha mwenzangu ambaye alisogea kwa nyuma badala ya kulikwepa matokeo yake likamgonga," alisema Bw. Mngazija na kuongeza kwamba alikwepa gari hilo likiwa limemfikia hatua mbili tu na kama siyo kuitwa kuelezwa gari kuja uswa wao, lingemgonga.


Mkuu wa wilaya ambaye alifika kwenye eneo hilo na baadaye kwenda hospitali kushughulikia tiba ya wanafunzi hao, alisema tukio hilo ni la kusikitisha na alishawahi kutoa taadhali kuhusu magari yanayokwenda kwenye sherehe kama hizo shuleni kwamba magari yaegeshwe kwenye maeneo maalum kuliko kuwekwa katika maeneo kama hayo ambayo yanaweza kutokea ajali kama hizo.


Wanafunzi hao, wamelazwa katika hospitali ya Magunga wilayani hapa wakiendelea kupatiwa matibabu huku mmoja wao Zahra akiwekewa mtambo wa kumuongezea kupumua Oksijeni na wengine hali zao zinaendelea vizuri. Mahafali yaliendelea lakini hayakuwa na furaha kutokana na tukio hilo.